Header Ads

test

JUBILEE WAZINDUA BIDHAA YA FBIZ KUWAFIKIA WAFANYA KAZI WALIOKO KATIKA KAMPUNI NDOGONDOGO

 

Na Said Mwishehe, Michuzi TV



KAMPUNI ya Jubilee Insurance imezindua huduma ya  bima ya FBiz  itakayokuwa ikihudumia wafanyakazi walioko katika Kampuni ndogo ndogo zenye wafanyakazi kuanzia watatu mpaka 15,lengo kuu la bidhaa hiyo ni kuwafikia wafanyakazi hao ambao wamekuwa wakihitaji kupata huduma za Kampuni hiyo.

Akizungumza leo Julai 29,2024 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa bidhaa hiyo ya FBiz ,Ofisa Undeshaji wa kampuni ya Jubilee Shaban Salehe amesema kuzinduliwa kwa bidhaa hiyo kunakwenda kulifikia kundi kubwa la wafanyakazi wanaofanyakazi katika Kampuni ndogo ndogo.

Amefafanua kuwa wanatambua kazi kubwa na nzuri wanayoifanya katika sekta ya afya katika upande wa huduma za bima na wanaunga mkono juhudi za Serikali za kutaka kila Mtanzania kuwa na bima ya afya.

Amesisitiza wao kama Jubilee wamekuja na bidhaa mpya ambayo itaziwezesha kampuni ndogo ambazo zinawafanyakazi kuanzia watu mpaka 15 wanapata bidhaa zao kupitia bima ya FBiz huku akibainisha huduma ambayo wameizindua leo inamachaguo mengi kuanzia chaguo la Sh.milioni 10 mpaka milioni 100.

"Tumeleta bidhaa hii kwasababu kumekuwa na mahitaji mengi sokoni na mahitaji haya yanatokea kwa vikundi mbalimbali vidogo vidogo.Bidhaa hii inakwenda kuhudumia kuanzia watu watatu na kuendelea ,tunataka wenye biashara ndogo ndogo wasione wameachwa na bima zetu,"amesema Salehe.

Pia amesema Jubilee wamekuwa wakifanya juhudi mbalimbali kuhakikisha wanapeleka kwa Wananchi bidhaa mbalimbali ambazo ziko katika  kuhakikisha zinatoa ufumbuzi wa matatizo ya Watanzania hasa zinazohusu sekta ya afya huku akisisitiza bidhaa zao zimefanikiwa kukubalika katika jamii na wanajivunia kwa kukubalika huko.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Biashara katika kampuni hiyo Gwakisa Mwankesa ameeleza kwamba bima hiyo imewalenga wafanyakazi waliokuwa katika Kampuni ambazo zimeajiri wafanyakazi wachache kuanzia watatu,wanne ,Watano mpaka 15 na huduma hiyo ni Maalumu kulingana na mahitaji.

Amefafanua huduma hiyo baada ya kuzinduliwa sasa itapatikana katika maeneo yote nchini kuwa Kampuni ya Jubilee iko kila mahali."Kupitia bima hii  itaruhusu mtu kupata huduma nchini Tanzania kwani tunayo bidhaa nyingine ambayo yenyewe imekuwa ikihudumia Afrika na India.

Awali Jacqline Mtei ambaye ni Ofisa kutoka kitengo hicho amesisitiza kwamba bima hiyo inawalenga watu kuanzia miaka 18 mpaka miaka 80 kwa wale ambao wako kazini pamoja na watoto wenye kuanzia umri wa miaka 0 mpaka miaka 23 kama wapo shuleni.

Katika hatua nyingine Valentino Mkenda ambaye ni  Meneja wa Mawakala Wadogo kutoka Kampuni ya Jubilee ametumia nafasi hiyo kuwashukuru Mawakala wote wanaofanyanao kazi kwani wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha bidhaa zao zinafika kwa Watanzania.





 

No comments