Header Ads

test

NYASA YAKUSANYA MAPATO KWA ASILIMIA 124.91

 

Na Albano Midelo


Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma imevuka lengo la ukusanyaji mapato,baada ya kufanikiwa kukusanya mapato ya zaidi ya shilingi bilioni 2.17 sawa na asilimia 124.91 katika kipindi cha mwaka 2023/2024.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Khalid Khalif kwenye kikao cha Baraza la madiwani cha kujadili taarifa ya Hesabu za mwisho za Halmashauri kwa mwaka wa fedha za 2023/2024 kilichofanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Mkurugenzi Kilosa Mbambabay.

Amebainisha kuwa kati ya makusanyo hayo,mapato halisi ni shilingi bilioni 1.32 na mapato kutoka katika vyanzo zuiliwa ni zaidi ya shilingi milioni 859.

“Fedha za miradi ya maendeleo ambazo zimepokelewa katika kipindi hicho ni 11,857,058,019 ambazo zimetumika kwa ajili ya mfuko wa afya wa Pamoja,elimu bure, TASAF, SEUIP, P4R, UNICEF,CDCF,chanjo ya polio, umaliziaji wa maboma, shule shikizi,BOOST na swash’’,alisema.

Ameongeza kuwa mapato kutokana na kodi mbalimbali katika kipindi hicho yameongezeka kutoka shilingi 202,319,610 kwa mwaka 2022/2023 hadi kufikia shilingi 271,856,574 mwaka 2023/2024.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mheshimiwa Peres Magiri akizungumza kwenye kikao hicho ameagiza kufanyika vikao vya kamati ya afya ngazi ya wilaya ambavyo vinazungumzia suala zima la afya kwa ujumla ikiwemo kutambua suala zima la virusi vya UKIMWI na vifo vya mama na mtoto.

Mkuu wa Wilaya pia ameagiza ratiba ya vikao vya lishe ngazi ya Halmashauri iandaliwe na kuhakikisha vikao vinafanyika kwa wakati ili kutekeleza mikataba ya lishe katika ngazi zote hadi Kata ili kukabiliana na udumavu.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Mheshimiwa Stewart Nombo amewapongeza watumishi na waheshimiwa madiwani wa Halmashauri hiyo kwa kusimamia ukusanyaji wa mapato hali iliyosababisha kuvuka malengo ya makusanyo kwa asilimia zaidi ya 124.

Baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa lina madiwani wa kuchaguliwa 20,viti ,maalum madiwani saba na Mheshimiwa mbunge mmoja.Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Mheshimiwa Stewart Nombo akizungumza kwenye kikao cha Baraza la madiwani la Hesabu za mwisho mwa mwaka 2023/2024 katika ukumbi wa Halmashauri hiyo Kilosa Mbambabay.Baadhi ya waheshimiwa madiwani wa Halmashauri ya Nyasa wakiwa kwenye kikao cha Baraza la madiwani Kilosa Mbambabay.Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mheshimiwa Peres Magiri akizungumza kwenye kikao cha Baraza la madiwani la Halmashauri ya Nyasa.Baadhi ya wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa wakifuatilia kikao cha Baraza la madiwani.

No comments