Header Ads

test

MNEC MFINANGA ATAKA WALIOHUJUMU MRADI WA MAJI KWA KUCHOMA MOTO MABOMBA KUSAKWA.

 

NA WILLIUM PAUL, SAME. 

MJUMBE wa Halmashauri kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa (MNEC) kupitia mkoa wa Kilimanjaro, Seleman Mfinanga amemtaka Afisa Tarafa wa Tarafa ya Gonja maore, wilayani Same, Kalua Muhunzi kuwatafuta wale wote waliohujumu mradi wa maji wa Mroyo-Kisangaze- Mpirani kwa kuyachoma moto mabomba ya maji yenye thamani ya 880,000 na kuwafikisha katika vyombo vya sheria. 

Mnec Mfinanga alitoa kauli hiyo leo alipotembelea kukagua mradi huo ikiwa ni Ukaguzi wa utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi kwa wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi mkoa wa Kilimanjaro. 

Alisema kuwa, haiwezekani serikali ipeleke fedha nyingi kwa ajili ya kutatua changamoto ya maji lakini baadhi ya watu wasio waaminifu wahujumu mradi huo kwa kuchoma moto mabomba waache kuchukuliwa sheria. 

"Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kwa vitendo kumtua mama ndoo kichwani lakini wapo baadhi ya watu kwa makusudi wanarudisha jitihada hizo nyuma hili haliwezi kukubalika nakuagiza Afisa Tarafa nenda mkawasake wale wote waliofanya hilo tukio maana wanafahamika na muwafikishe katika vyombo vya sheria" Alisema Mfinanga. 

Katika hatua nyingine, Kiongozi huyo ameiagiza Wakala wa maji mjini na vijijini, Ruwasa kuhakikisha ifikapo Oktoba 15 mwaka huu maji yawe yameshafika katika kijiji cha Makokane. 

Awali akisoma taarifa za mradi huo, Meneja wa Ruwasa wilaya ya Same, Mhandisi Abdallah Gendaeka alisema kuwa mradi huo unagharimu Bilioni 1.6 ambapo utekelezaji wake ulianza mwezi Februari mwaka huu. 

Mhandisi Gendaeka alisema kuwa, mradi huo umelenga kutoa huduma katika vijiji vya Mpirani kata ya Maore na kijiji cha Makokane kata ya Kalemawe ambapo jumla ya wakazi 6826 watanufaika nao. 

Alisema kuwa, changamoto waliyonayo katika mradi huo ni uharibifu wa mabomba 20 ya inchi nne yenye thamani ya 880000 yalichomwa moto na wakazi wa kata ya Lugulu ambapo pia wapo wananchi wamekuwa wakikata mabomba kwa makusudi. 








 

No comments