Header Ads

test

OCPD yawanoa Waandishi wa Sheria kukabili mahitaji ya Taifa.

 

 Na: Calvin Gwabara – Dodoma.

Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria (OCPD) imeendelea kuwekeza katika kuwaendeleza watumishi wake kitaaluma kwa kuwapatia fursa za mafunzo ndani na nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye weledi, utaalamu wa kisekta na uwezo wa kuandaa sheria bora zinazowezesha utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali.

Mwandishi Mkuu wa Sheria (CPD) Bwana Onorius John Njole wakati akiongea na Mwandishi wetu kuhusu mpango huo wa mafunzo.

Hayo yamebainishwa na Mwandishi Mkuu wa Sheria (CPD) Bwana Onorius John Njole wakati akiongea na Mwandishi wetu kuhusu jitihada zinazochukuliwa na ofisi yake katika kuiwezesha nchi kupata sheria bora zinazokwenda na wakati.

Bwana Njole amesema Uandishi wa Sheria ni taaluma maalumu yenye misingi, kanuni na viwango vyake, hivyo inahitaji mafunzo mahsusi na uwekezaji endelevu katika kujenga uwezo wa wataalamu.

“Ingawa Waandishi wa Sheria ni Wanasheria, si kila Mwanasheria ni Mwandishi wa Sheria mtu anakuwa Mwandishi wa Sheria baada ya kupata taaluma maalumu ya uandishi wa Sheria,” amesema Njole.

Amesema mkakati wa Ofisi hiyo haujajikita katika kuwafundisha waandishi namna ya kuandika sheria pekee bali pia kuwajengea utaalamu katika sekta ambazo sheria wanazoandika zinalenga kuzisimamia kwa kuwa uelewa huo huwasaidia kutambua mahitaji halisi ya sekta na kuandaa sheria zinazoweza kutatua changamoto na kuwezesha utekelezaji wa mipango ya Taifa.

Mwandishi huyo Mkuu wa Sheria amesema kwa kutambua umuhimu wa taaluma hiyo, Ofisi ya Mwadishi Mkuu wa Sheria (OCPD) imekuwa ikiwapeleka watumishi kupata mafunzo katika vyuo na taasisi mbalimbali ndani na nje ya nchi zilizobobea, huku baadhi wakipata utaalamu katika maeneo mahsusi kama Kodi, Sheria za Bahari na Uandishi wa Sheria.

Aidha amesema kuwa OCPD pia imeweka mkazo katika mafunzo ya ndani kwa kuwa sehemu kubwa ya uandishi wa sheria hujifunzwa kupitia utekelezaji wa majukumu ya kila siku. Ofisi hiyo imekuwa na mfumo wa kufundishana baina ya waandishi wa sheria, ikiwemo madarasa ya maeneo mbalimbali ya uandishi wa sheria yanayofanyika kila Jumatatu.

“Katika mwaka uliomalizika, Waandishi wawili walipelekwa Chuo cha West Indies, wengine tisa Chuo cha Sheria cha Zambia kwa ajili ya mafunzo ya uandishi wa sheria, huku mpango wa mwaka 2026 ukilenga kupeleka waandishi wengine wawili Zambia na wawili katika Chuo cha Sheria cha London” alieleza Njole.

Aliongeza “Uwekezaji huu pia unalenga kuwa na wataalamu wenye utaalamu wa kisekta, ambapo katika mwaka uliomalizika waandishi wawili walipata shahada za uzamili katika eneo la kodi, huku waandishi wanne wakipata shahada za uzamili katika Sheria za Bahari nchini Malta”.

Mwandishi huyo Mkuu wa Sheria alisema lengo la muda mrefu ni kuhakikisha Tanzania inakuwa na wataalamu wa kutosha katika uandishi wa sheria wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya ndani na pia kutoa huduma za uandishi wa sheria katika nchi nyingine, hususan ndani ya Jumuiya ya Madola.

Miongoni mwa wanufaika wa mpango huo ni Boniphas Mondu Giabe aliyepata fursa ya kusoma Shahada ya Uzamili katika Uandishi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha West Indies, Kampasi ya Cave Hill, nchini Barbados ambaye amesema mafunzo hayo yamemsaidia kuongeza ujuzi katika Uandishi wa Sheria na kumjengea uelewa wa umuhimu wa kuandaa sheria kwa lugha inayoeleweka kwa urahisi na inayozingatia misingi ya kikatiba na haki za binadamu.

Baadhi ya Watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mahafali yaliyofanyika katika Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO International Maritime Law Institute – IMLI), nchini Malta.

“Moja ya mambo muhimu niliyojifunza ni kwamba sheria zinapaswa kuandikwa kwa lugha na mtindo unaowawezesha watumiaji kuzielewa kwa urahisi lakini pia zinapaswa kuzingatia misingi ya kikatiba pamoja na haki za binadamu,” amesema Giabe.

Amesema maarifa aliyoyapata katika maeneo ya sheria za utawala, sheria za katiba, mafuta na gesi yanaendelea kumsaidia katika utekelezaji wa majukumu yake, huku akishirikisha ujuzi huo na waandishi wengine wa sheria katika kuandaa sheria bora na zinazotabirika.

Nae mnufaika mwingine Bi. Loveness Jacob aliyepata ufadhili wa Shahada ya Uzamili katika Sheria za Kimataifa za Baharini kutoka Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO International Maritime Law Institute – IMLI), nchini Malta, ambapo amesema mafunzo hayo yamemwongezea utaalamu katika eneo muhimu la kimkakati kwa Serikali na Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.

“Utaalamu nilioupata utasaidia katika uandaaji wa Sheria zinazotokana na mikataba ya kimataifa ya baharini, uandaaji wa nyaraka za utekelezaji wa mikataba hiyo na kuimarisha usimamizi wa masuala ya bahari na kuchangia katika kukuza uchumi wa buluu kupitia uandishi wa sheria za sekta hiyo, alisema Jacob.

Amesema mafunzo hayo pia yamempa fursa ya kupata uzoefu wa vitendo katika masuala ya sheria za kimataifa kupitia ushiriki katika mkutano wa Kamati ya Kisheria ya Shirika la Kimataifa la Bahari (IMO Legal Committee) ambapo alijifunza namna nchi zinavyoshiriki katika mijadala ya kimataifa na kuwasilisha hoja za kisheria.

Aidha kwa upande wake Bi. Winfrida Mwera ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Uandishi na Ufasiri wa Sheria Ndogo katika OCPD, aliyepata fursa ya kusoma Postgraduate Diploma in Legislative Drafting, kwa lengo la kuimarisha uwezo wake katika kuandaa na kurekebisha miswada ya sheria, amesema mafunzo hayo yamemwongezea ujuzi katika matumizi ya mbinu na misingi mbalimbali ya uandishi wa sheria, pamoja na uwezo wa kuandaa sheria zilizo wazi, sahihi na zenye ufanisi.

“Nitatumia ujuzi na maarifa niliyoyapata kupitia mafunzo haya katika kuandaa rasimu za sheria zenye ubora wa juu, kupunguza mapungufu katika uandishi wa sheria na kutoa mchango wenye tija katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya OCPD,” amesema Mwera.

Amesema uwekezaji huo umechangia kuongeza uwezo wa watumishi na kuboresha utendaji wa taasisi huku akitoa wito wa kuendelea kutolewa kwa fursa za mafunzo kwa wataalamu wengine.

Katika kuhakikisha mafunzo wanayoyapata kutoka ndani na nje ya nchi Ofisi hiyo ina siku maalumu kila wiki kwa wahitimu kukutana na watumishi wenzao na kuwafndisha na kujengeana uwezo kupitia mafunzo ya ndani ili wote wanufaike na kuchangia ubora wa kazi za ofisi kwa maslahi mapana ya Taifa.

Mwandishi wa Sheria kutoka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria chini akifurahia mara baada ya kupokea tuzo kwa kufanya vizuri zaidi kwenye eneo la Sheria za Bahari wakati wa mahafali kutoka Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO) nchini Malta.  

m



No comments