Header Ads

test

WIZARA YA MALIASILI YAPEWA TANO KWA UBUNIFU MAONESHO YA NANENE KITAIFA DODOMA

 

Na. John Bera – DODOMA 


Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kuonyesha umahiri wake katika Maonesho ya Nane Nane yanayofanyika eneo la Nzuguni, Jijini Dodoma. Wananchi wamekuwa wakivutiwa na Banda la Wizara hiyo ambapo wanaweza kujionea vivutio mbalimbali vya utalii ikiwa ni pamoja na wanyamapori hai.

Akizungumza baada ya kutembelea Banda hilo, Elias Majula, mkazi wa Chidachi Dodoma, amepongeza Wizara hiyo kwa kuonesha vivutio mbalimbali vya utalii katika Banda hilo. Amefurahishwa hasa na uwepo wa wanyamapori adimu kama Chui, ambao wanaweza kuonekana moja kwa moja katika banda hilo.

"Napenda kuwapongeza sana Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuleta vivutio hivi. Banda hili limekuwa ni la kipekee sana. Watoto wangu pia wamefurahia sana. Nawasihi watu wote waliopo Dodoma na mikoa jirani kufika katika banda hili ili waweze kujionea vivutio mbalimbali vya utalii, hasa wanyamapori adimu kama chui," amesema Bw. Majula.

Moja ya waratibu wa maonesho hayo, Bw. William Mwita amesisitiza kuwa Wizara itaendelea kuwa na ubunifu ili kuwafurahisha wananchi. Wataendelea kuonesha vivutio vyenye umuhimu kwa  wananchi pamoja na fursa za uwekezaji na ajira zinazotokana na uhifadhi wa maliasili, malikale na uendelezaji wa utalii  lengo ikiwa ni kuhakikisha kuwa rasilimali za Taifa zinaendelea kuwapunguzia wananchi umasikini na kuwapatia furaha wanapofika katika mabanda hayo.












 

No comments